Ukiwa nao waambie, maneno yawafikie,
Jitahidi wasikie, ujumbe uwafikie,
Ili wasiulizie, bure wasijisumbue,
Waambie hao wote, umenichagua mie.
Wakate vyao vilimi, ikibidi waumie,
Sema wanipenda mimi, waambie wasikie,
Sema mara kumi kumi, sauti iwafikie,
Waambie hao wote, kuwa wanipenda mie.
Hawapendi ninajua, we’ waache waumie,
Wivu unawasumbua, watamani watibue,
Sie tunaomba dua, Muumba atujalie,
Waambie hao wote, umenichagua mi.
Waambie wafitini, na chuki zao walie,
Na wala wasijihini, hawatotuweza sie,
Tumeshazama dimbwini, tumeshanogewa sie,
Waambie hao wote, kuwa wanipenda mie.
We’ waambie mpenzi, yawachome waumie,
Na zidisha kunienzi, ili nifaidi mie,
Niyafaidi mapenzi, pendolo nijivunie,
Waambie hao wote, umenichagua mie.
Mpenzi we’ u mzuri, yeyote asikwambie,
Unanipa ufahari, na raha usisikie,
Nasi twombeane kheri, mapenzi yetu yakue,
Waambie hao wote, kuwa wanipenda mie.
This poem has not been translated into any other language yet.
I would like to translate this poem