Huba Poem by Fadhy Mtanga

Huba

Nijaze mie mahaba,
Ili nile nikashiba,
Nipe mapenzi ya huba,
Nitosheke na dunia.

Nipe chakula kitamu,
Kinijaze mi’ wazimu,
Kinipandishe stimu,
Nibaki sikilizia.

Nigee mapenzi yote,
Yaniingie nidate,
Raha kamili nipate,
Raha isiyopungua.

Niambie wanipenda,
Siposema nitakonda,
Hata homa kunipanda,
Moyoni nikaumia.

Nifanye nifurahie,
Katu mi’ nisiumie,
Mapenzi nijivunie,
Na raha kujisikia.

Nipe mimi peke yangu,
Usimpe na mwenzangu,
Umeumbwa uwe wangu,
Mungu amenipatia.

Kunipenda usichoke,
Wanifanya niridhike,
Na moyo uburudike,
U wangu najivunia.

COMMENTS OF THE POEM
READ THIS POEM IN OTHER LANGUAGES
Fadhy Mtanga

Fadhy Mtanga

Dar es Salaam, Tanzania
Close
Error Success