Keshachoka Usukani Poem by Abdallah Mpogole

Keshachoka Usukani

Hapo mwanzo tuliona, nia yake ilikwepo.
Imani tulijazana, hakuachwa mtu hapo.
Pamoja tulipendana, wakanza badili upepo.
Babu kaanza kuchoka, ashindwa shika sukani.

Ikaja ile awamu, aso mwana hana lake.
Ruksa ilo timamu, mtu achukue chake.
Ikawa kama karamu, chombo dirani kitoke.
Babu asahau zama, ajifanya yu kijana.

Macho manne ajongea, aja kiteknolojia.
MV Bukoba kalia, chozile kawamwagia.
Wakaja wana ubia, kichwakichwa kuingia.
Babu apotea njia, shimoni twadidimia.

Babu kamleta wa pwani, ati aongeze kasi.
Gaidi sera nchini, milipuko na risasi.
Akatinga mpirani, mapanki yalimghasi.
Kakosa nini Dereva, eti ni bahati mbaya!

Vita ikawa fisadi, walaji wako makundi.
Wote wakawa baridi, umeme wa Richimondi.
Achia ngazi yabidi, wakaburuzwa wahindi.
Babu wanao wa benki, pia nao wasaliti?

Hivi sasa ni kihoro, wao kwa wao walana.
Tulisubiri wa Moro, hukumu kosa hakuna.
Katika kiza totoro, wanyonge haki hawana.
Jigeuze yako rangi, ulonayo ishachoka.

Kama vipi asiachwe, mla chumvi wa kijani.
Hachezi ila abebwe, kazoea wamezani.
Wamemtema vikongwe, na vitoto vya shuleni.
Hawa wote si wajinga, mvi zako si busara.

Napenda kukwandikia, sidhani kama waona.
Jaribu kudurusia, ukifata weza pona.
Huwezi demokrasia, japo wajisifu sana.
Umepoteza pambio, nchi yetu kimbilio.

COMMENTS OF THE POEM
READ THIS POEM IN OTHER LANGUAGES
Abdallah Mpogole

Abdallah Mpogole

Iringa, Tanzania
Close
Error Success