Kusubiri nimechoka, na muda wazidi kwenda,
Mwenzio nataabika, mwili wazidi kukonda,
Raha iliniponyoka, wewe mbali umekwenda,
Urudi basi mpenzi, nakungojea kwa hamu.
Nakungojea kwa hamu, siku utakayorudi,
Unipe mashamshamu, kwani u wangu waridi,
Mapenzi yako matamu, nipate kuyafaidi,
Kwani nimekuchagua, mwingine simtamani.
Mwingine simtamani, nd'o maana nakungoja,
U ndani mwangu moyoni, wewe pekee mmoja,
Wewe huna kifani, urudi tuwe pamoja,
Ona nachanganyikiwa, natamani kukuona.
Natamani kukuona, wewe unipaye raha,
Vinginevyo raha sina, nitakosa hata siha,
Juwa nakupenda sana, wewe u yangu furaha,
Mpenzi usikawie, bure nitamwaga chozi.
Bure nitamwaga chozi, kukuona nikikosa,
Peke yangu sijiwezi, penzi lako lanitesa,
Rudi wangu laazizi, unipaye mi' hamasa,
Nangoja leo na kesho, fanya urudi mapema.
Fanya urudi mapema, upweke wanielemea,
Jitahidi fanya hima, urudi kuniokoa,
Nisije kupata homa, na kuzidi kuumia,
Tabibu wangu ni wewe, rudi ili unitibu.
Rudi ili unitibu, maradhi ya moyo wangu,
Maradhi yan'onisibu, ni wewe mpenzi wangu,
Wewe u wangu muhibu, shahidi yangu ni Mungu,
Mpenzi usichelewe, homa itanizidia.
Homa itanizidia, endapo utachelewa,
Hivyo nakusubiria, raha nataka kupewa,
Useme nikasikia, kwamba hima utakuwa,
Umekuja kunitibu, kabla sijatibuka.
This poem has not been translated into any other language yet.
I would like to translate this poem