Alaa Kumbe! Poem by Fadhy Mtanga

Alaa Kumbe!



Asubuhi waamka,
Waanza kukuna kichwa,
Unawaza,
Utawaza sana!
Ukipata jawabu,
Heko nyingi.

Jana,
Hukuyamaliza yalojiri,
Ungeyamaliza vipi?
Uwezo hukuwa nao,
Kwa nini?
Najua huna jibu.

Maisha!
Kwani ni nini?
Ama yana nini?
Utawaza sana,
Nami nawaza sana,
Ala kumbe?
Kumbe nini?

Wajiuliza mara mia,
Uwape tena?
Lipi jipya litakuja?
Ngoja kidogo.
Maisha, maisha,
Yanakwisha,
Usiseme hivyo,
Nisemeni?
Sijui.
Hayo madaraka,
Tumewapa,
Wengine wakachukua bila kupewa,
Nini chanzo?
Pengine tamaa.
Tulikuwa na matarajio,
Eti eh!

Matarajio?
Ya nini tena,
Kwenu hamli?
Hapana.
Sasa nini?
Hali bora.

Alaa kumbe!
Ikawaje sasa?
Hatuhitaji kukujibu,
Maana hali yenyewe,
Mwenyewe si unaiona?

Hapana sioni kitu,
Ni kweli,
Huoni kitu ingawa una macho,
Machoyo mapambo,
Huwezi ona lolote,
Kwa kuwa,
Hupendi kufanya jitihada,
Jitihada? Za nini tena?
Katika kufikiri.

Mmh!
Sote tukaguna.

COMMENTS OF THE POEM
READ THIS POEM IN OTHER LANGUAGES
Fadhy Mtanga

Fadhy Mtanga

Dar es Salaam, Tanzania
Close
Error Success